Kamati ya Mwenge ya Wilaya ya Hanang’ imefanya ziara ya kukagua miradi ya maendeleo inayotarajiwa kupitiwa na Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2025. Ziara hiyo imeongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Hanang’, Mheshimiwa Almishi Hazali.
Katika ukaguzi huo, Kamati ilitembelea miradi kadhaa inayotekelezwa kwa lengo la kuleta ustawi wa jamii, ikiwa ni pamoja na sekta za afya, elimu, maji, na miundombinu. Miradi hiyo inatarajiwa kuoneshwa kwa umahiri wakati wa mapokezi ya Mwenge wa Uhuru, kama alama ya juhudi za Serikali ya Wilaya katika kuwaletea wananchi maendeleo.
Akizungumza baada ya ukaguzi huo, Mheshimiwa Hazali alieleza kuridhishwa kwake na hatua ya utekelezaji wa miradi hiyo, akisema kuwa inadhihirisha namna viongozi na wananchi wa Hanang’ walivyojipanga kuhakikisha mwenge unapita katika miradi iliyokamilika na yenye manufaa ya moja kwa moja kwa jamii.
Aidha, Mkuu huyo wa Wilaya alitoa wito kwa wasimamizi wote wa miradi kuhakikisha wanatunza vyema nyaraka muhimu zinazohusu miradi hiyo, ikiwa ni pamoja na mikataba, risiti, picha na taarifa za maendeleo kwa kila hatua ya utekelezaji. Alisisitiza kuwa utunzaji bora wa kumbukumbu si tu kwa ajili ya ukaguzi wa Mwenge, bali ni kwa lengo la kuwajibika kwa wananchi na mamlaka nyingine za kiserikali.
“Miradi yote, iwe inapitiwa na Mwenge wa Uhuru au la, inapaswa kusimamiwa kwa uadilifu na uzalendo. Tunapaswa kuonesha uwajibikaji kwa fedha za umma kwa kila hatua ya utekelezaji,” alisema Mheshimiwa Hazali.
Ziara hiyo ya Kamati ya Mwenge ni sehemu ya maandalizi muhimu kuelekea Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2025, na Serikali ya Wilaya imeweka mkazo mkubwa katika kuhakikisha miradi yote inayotekelezwa ina tija na inatekelezwa kwa kuzingatia thamani halisi ya fedha.
Hanang' District Council Headquater located at the Northern part of Katesh town in Ganana Ward
Postal Address: P.O Box 02 Katesh-Hanang'
Telephone: 027-2530022 / 42
Mobile: +255 762 362 950
Email: ded@hanangdc.go.tz
Copyright ©2016 GWF . All rights reserved.